Wasanii wa filamu 10 waliofanya vizuri mwaka 2014
Bongo5 ikishirikina na wasambazaji na wauzaji wa filamu, inakuletea orodha ya waigizaji 10 waliofanya vizuri mwaka 2014.
Salim Ahmed aka Gabo
Mwaka jana msanii huyu alitamba na filamu ya ‘Bado Natafuta’ ambayo bado inaendelea kufanya vizuri sokoni. Mwaka huu Gabo pia ameonekana kwenye filamu nyingi ikiwemo ‘Siri Ya Giningi’ iliyofanya vizuri sokoni akishirikiana na Sabby Angel pamoja na Mzee Korongo. Kinachomfanya muigizaji huyu apendwe ni ule uwezo wake wa kubeba uhusika.
Shamsa Ford
Mwaka jana Shamsa alihit na filamu ya Bado Natafuta akiwa na Gabo. Mwaka huu ameweza kutikisa tena kwa mauzo ya filamu yake ya Chausiku inayodaiwa kufikia rekodi ya mauzo iliyowekwa na marehemu Steven Kanumba kupitia filamu yake ya mwisho, Ndoa Yangu.
Jacob Stephen aka JB
Mwaka huu, mmiliki wa Jerusalem Films na muongozaji wa filamu nyingi zinazozalishwa na kampuni hiyo, JB ametamba na filamu kama ‘Hukumu ya Ndoa’ na ‘Mikono Salama’ambazo aliziongoza pia. Filamu zingine alizoziongoza ni pamoja ‘Wageni Wangu’ pamoja na ‘Chausiku’.
Salma Jabu aka Nisha
Nisha ambaye amewahi kutamba na filamu kama Tikisa, Pusi na Paku mwaka huu mwanadada huyo aliachia filamu ya komedi, Zena na Betina inayofanya vizuri sokoni.
Jacqueline Wolper
Pamoja na hivi karibuni kuiambia Bongo5 kuwa bado yupo benchi kucheza filamu zake binafsi kutokana na mapato kuwa finyu, mwaka huu alitoka na filamu ya Tom Boy. Pia ameokana kwenye filamu ya VIP iliyoingia sokoni October.
Irene Uwoya
Mwaka huu Irene ameonekana kwenye filamu kama JAMAL na Nesi Bandia ambazo zote zimefanya vizuri sokoni.
King Majuto
Mzee Majuto anaendelea kufanya vizuri sokoni kutokana na filamu kama Duplicate, Chungu Kimoja, Nahama na zingine.
Vincent Kigosi aka Ray
Ray kupitia kampuni yake, RJ Company ameendelea kufanya vizuri na hivi karibuni aliachia filamu ya VIP akiwa na Wolper Salha na wengine.
Cloud
Cloud ameendelea kufanya filamu zenye visa vya kuvutia kama Fundi Selemala na Doctor Max zilizotoka mwaka huu.
Ringo na Tin White
Hii ni timu ya watu wawili. Wasanii hawa wa vichekesho wanapendwa sana na hata kazi zao zinapoingia sokoni huuza vyema. Mwaka huu walitoa filamu kama Utani na 4 Days Mission.