Habari

Wapiga dili TPA kuchukuliwa hatua

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imesema itawachukulia hatua watumishi wa mamlaka hiyo wanaojishughulisha na michezo michafu wakishirikiana na wafanyabiashara katika minada inayofanyika bandarini.

Akizungumza katika mahojiano ya moja kwa moja na kituo cha redio jana, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Deusdedit Kakoko amesema hatua ambazo atachukua ni pamoja na kupiga mnada mali za wahusika wote ambao watabainika kuhusika katika mchezo huo mchafu.

“Katika Serikali ya Awamu ya Tano ni vizuri kufuatilia utendaji, kilichozungumzwa tumekisikia na tuko tayari kuchukua hatua za haraka kwa kinachozungumzwa,” alisema Kakoko.

Kakoko amesema anatambua kuwa kuna minada inafanyika katika Bandari ya Dar es Salaam kwa mizigo ambayo hushindwa kulipiwa ndani ya muda uliowekwa kisheria, lakini hakuwa na taarifa ya njama zinazofanywa na baadhi ya wafanyakazi wa TPA ambao sio waaminifu, “Kama tukipata taarifa za kina tutachukua hatua mara moja,” alisema.

Kwa mujibu wa mtoa taarifa hiyo ambaye ni mdau wa bandari, kuna ujanja unaofanywa na baadhi ya wafanyakazi ambao wanaagiza mzigo kutoka nje, wanalipia asilimia chache kwa makubaliano kwamba mzigo huo utakapofika bandari ya Dar es Salaam atamalizia fedha zilizobaki.

Lakini wafanyabiashara hao matokeo yake wakifikisha mzigo hapa nchini badala ya kulipa fedha zilizobaki wanachelewesha kulipia mzigo mpaka muda unapita wa kuhifadhi mzigo bandarini na mzigo huo kupigwa mnada.

Aidha, mchezo huo mchafu hufanywa na wafanyakazi wasio waaminifu wa TPA kwa kushirikiana na wafanyabiashara kisha mzio anauziwa kwa bei ya chini ambapo bila kulipa fedha ambayo mfanyabiashara alikuwa amebakiza deni alikochukulia mzigo jambo ambalo linachafua jina la bandari ya Dar es Salaam.

BY: Emmy Mwaipopo

Chanzo: Habari Leo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents