Habari

Wanaosomea diploma nao kuanza kunufaika mkopo wa HELSB

Serikali imewasilisha pendekezo la mabadiliko ya Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ili kuwezesha wanafunzi wanaochukua Stashahada katika vipaumbele vya kitaifa, kupewa mikopo ya kuwawezesha kuchukua elimu husika.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako alisema mabadiliko hayo, yamelenga kuwezesha kasi katika uchumi wa viwanda.

Profesa Ndalichako alisema mabadiliko katika Sheria Namba 4 ya Mwaka 2016 ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), yamelenga kutoa nafasi ya kada ya Stashahada inayohitajika ambao wamekuwa hawapati mikopo.

“Kwa lengo la kupata balance (mizania) na kwa kuwa Diploma nayo iko kwenye elimu ya juu, watoto ni wale wale. Kuna wengine nao wanashindwa kumudu gharama na ili serikali ipate uwiano mzuri tumeona ni vizuri kuwe na marekebisho ya sheria,” alieleza Profesa Ndalichako.

Profesa Ndalichako alisema kuna umuhimu mkubwa wa kada ya Stashahada, hasa wanaokwenda sanjari na vipaumbele vya kitaifa kwenye msukumo wa Serikali ya Awamu ya Tano wa ujenzi wa taifa la vijana, kama ilivyo kwa wenye Shahada.

“Kama taifa tunazungumzia uchumi wa viwanda,wadau wote hata wale wa ngazi ya kati ni muhimu katika kuhakikisha kwamba ajenda hii inafanikiwa kama vile ambavyo wale wa digrii wangelifanya,” aliongeza waziri huyo.

Mwaka 2004, kulikuwepo na mabadiliko katika sheria hiyo iliyowezesha wanaochukua masomo ya sayansi, hisabati na elimu ya msingi (kwenye msisitizo wa sayansi na hisabati), kupata mikopo ya elimu, nafasi iliyoanza kutumika mwaka 2014, lakini hatua hiyo ilisimamishwa wakati wa muhula wa masomo wa mwaka 2016/17.

Hata hivyo, HESLB ilikaririwa ikisema kwamba maamuzi ya kusitisha utoaji wa mikopo, ililenga kutekeleza maagizo ya serikali. Hata hivyo, jana Profesa Ndalichako alisema kwamba uamuzi wa kusimamisha mikopo hiyo,ulitokana na nia ya serikali kufanya mabadiliko katika sheria hiyo ili kuipa wigo mpana zaidi kuliko kujikita katika eneo la sayansi pekee.

BY: Emmy Mwaipopo

Chanzo:Habari Leo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents