Habari

Vifaa vya kuhakiki vyeti ‘feki’ na kuandikisha Vitambulisho vya Taifa vyaibiwa

Vifaa vinavyotumika kuhakiki vyeti kwa watumishi wa umma pamoja na kuandikisha Vitambulisho vya Taifa, ikiwemo kamera zenye thamani ya Sh. milioni sita vimeibiwa na watu wasiojulikana katika jengo la ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.
p1-katuni_0

Kamera mbili na viegesho vyake (stand), vimebainika kupotea jana asubuhi wakati wa kujiandaa kuendelea na kazi ya kuhakiki vyeti na kuandikisha Vitambulisho vya Taifa.

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani humu, Nyabaganga Talaba, alithibitisha kupotea kwa kamera hizo za Nida.

“Leo (jana) asubuhi, Ofisa wa Nida alibaini kuwa kamera mbili na viegesha vyake, havionekani. Tunaendelea kufanya uchunguzi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kuwabaini wahusika na kuvipata vifaa hivyo,” alisema Talaba.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Stephen Magoiga pia alilithibitishia Nipashe kupotea kwa kamera mbili na viegesha vyake vilivyokuwa vimehifadhiwa kwenye ofisi ya halmashauri yake kwa ajili ya kupigia picha za Vitambulisho vya Taifa.

Hata hivyo, Magoiga alisema bado hajawapata undani zaidi kuhusu upotevu wa vifaa hivyo na watatoa taarifa kamili baadaye.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Muliro Jumanne Muliro, naye alithibitisha kutokea kwa tukio hilo la upotevu wa vifaa hivyo na kusema kuwa uchunguzi unaendelea.

“Vifaa hivi vinatumika kuandikisha Vitambulisho vya Taifa kazi inayoenda sambamba na uhakiki wa yeti kwa watumishi wa umma, vifaa havionekani, lakini tunaendelea na uchunguzi juu ya tukio hili ili kujua kama kuna wizi au la na mpaka sasa tumeshanahoji baadhi ya watu”, aliongeza Kamanda Muliro.

Source: IPP Media

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents