Video: Nikistaafu, nitapenda kuupanda mlima Kilimanjaro – Obama
Rais wa Marekani, Barack Obama amesema pindi akimaliza muhula wake wa pili, atapenda kuja Tanzania kwa mara ya pili na kuupanda mlima Kilimanjaro.
Obama alisema hayo juzi kwenye mahojiano exlusive na kituo cha redio cha Capital FM cha Kenya. Mtangazaji wa kituo hicho, Olive Burrows alimuuliza swali la ni maeneo gani anayopenda kutembelea kipindi akienda Kenya kama raia wa kawaida na Obama kusema angependa kutembelea mbuga za Masai Mara na Serengeti pamoja na kwenda kuukwea mlima mrefu zaidi barani Afrika, Kilimanjaro.
“Sio tu Kenya lakini kuna mazingira ambayo yameungana kutoka Uganda kwenye Tanzania. Kuupanda Mlima Kilimanjaro kinaonekana kama kinatakiwa kuwa kwenye orodha ya vitu vya kufanya pindi nikiondoka [madarakani],” alisema Obama.
“Secret Service kwa kawaida hawapendi mimi kupanda milima lakini kama raia wa kawaida bila shaka naweza kufanya kitu kama hicho,” aliongeza.
Obama alikuwa nchini Kenya kwenye ziara ya siku tatu kabla ya jana kuelekea jijini Addis Ababa, Ethiopia.