Videos

Video: Nape Nnauye atishiwa bastola kwenye mkutano na waandishi wa habari, asema hana kinyongo na uamuzi wa Rais

Aliyekuwa waziri wa habari,utamaduni, sanaa na michezo, Nape Nnauye Alhamis hii alilazimika kuzungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam akiwa amesimama juu ya gari nje ya ukumbi wa Protea Hotel baada ya polisi kutaka kuuzuia mkutano huo usifanyike.

Akiwa amezungukwa na kundi kubwa la waandishi wa habari, Nape alilaani kitendo cha askari kumnyooshea bunduki wakati alipokuwa akijiandaa kuzungumza na waandishi wa habari.

“Kwanini mnatoa bunduki hadharani, mimi jambazi?” alihoji.

“Nataka waliokuja kuzuia mkutano waambie kwanini wanazuia mkutano. Wanatoa bunduki hadharani, wanataka sasa nifanye nisivyowaza kufanya. They want to kill me. Nataka hawa waliotoa bunduki kwenye nchi huru waseme aliyewatuma kutoa bunduki hadharani, aliyetuma kuzuia mkutano, I want this kabla sijaingia kwenye gari kuondoka, tusifanyiane mambo ya kijinga nchi huru hii. Nimepigana mimi kutafuta kura za CCM halafu wanakuja wapuuzi wachache.”

Baada ya vuta ni kuvute na waandishi wa habari waliomtaka aanze kuzungumza, Nape alipanda juu ya gari lake huku akisisitiza kuwa yeye ni mwanahabari anayepigania uhuru wa wanahabari.

Kwenye hotuba yake Nape amesisitiza kuwa nia ya mkutano wake ulikuwa ni wa kuwaeleza watanzania kuwa nchi lazima iendelee na kuviovya vyombo vya usalama kutenda haki. Amesisitiza kuwa hana kinyongo na kutenguliwa kwa uteuzi wake huku akisisitiza kuwa vijana hawana cha kuogopa zaidi ya uoga wenyewe akiendelea kuweka mkazo tukio la kuwekea bastola ya kumtisha.

“Do you know how we fought for this country? Unajua nimeenda miezi 28 nalala porini. Nimepigana kuirudisha CCM madarakani anakuja mpuuzi mmoja anatoa bastola hapa.”

Amesisitiza kuwa yeye ni mtu mdogo kuliko nchi na kwamba Tanzania lazima iangalie inapokwenda.

“Nimekuwa mzalendo kwa nchi yangu, nimekuwa muungwana kwa nchi yangu na ninaapa kuendelea kuwa muungwana kwa nchi yangu, hilo hakuna atakayelibadilisha. Lakini mimi nimekuwa mzalendo kwa CCM ambayo niliikuta kwenye shimo inakwenda nikasimama kuinunua, watanzania wanajua,” alisisitiza.

Mheshimiwa Nape alisisitiza kuwa siku zote atasimamia katika ukweli na kile anachokiamini, kitu ambacho alifundishwa na marehemu baba yake, Mzee Moses Nnauye na kudai kuwa kama anachokiamini kikileta matatizo hatoteteleka.

“Mbegu ya kusimamia kwa hakika itaota,” aliweka mkazo.

Nape amemshukuru Rais Dkt John Magufuli kwa kumwamini katika wadhifa huo aliodumu kwa mwaka mmoja na pia kumpongeza Dkt Harrison Mwakyembe ambaye amewataka waandishi wa habari kumuunga mkono.

“Ninajua wapo ambao kwa namna moja ama nyingine wameumia, ninawaomba kama mimi mnayeniamini niko hapa kuwaambieni mambo yako sawa maisha lazima yaendelee naombeni mnisikilize, tuitulize nchi.”

Nape amewataka waandishi wa habari kuendelea kufanya kazi kwa kusimamia kwa wanachokiamini bila kuwa na uoga.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents