Ushirikiano huu wa Afrika Mashariki ndio njia pekee ya kula sahani moja na Wanaijeria!
Kwa mtazamo wetu, Afrika Mashariki haijawahi kuwa na ushirikiano wa karibu kama tunaouona sasa. Hebu tuangalie kwa ufupi.. Turudi nyuma hadi pale Victoria Kimani alipowashirikisha Diamond Platnumz na Ommy Dimpoz kufanya wimbo Prokoto.
Shaa alichaguliwa na kituo cha Citizen TV kuwa host wa show yao ya Sakata Mashariki na kiukweli watazamaji wamempokeza vizuri.
Shaa huyo huyo pia amefanya collabo na Redsan na mambo mengi yanakuja ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kufanya ngoma na Jacky Chandiru wa Uganda.
Hivi karibuni tumeshuhudia picha za wasanii wa Afrika Mashariki wakiwemo Shaa, AY, Maurice Kirya, Jose Chameleone, Nameless, Rabbit, Erick Wainaina na wengine walikutana jijini Nairobi ambako kuna kitu kikubwa kinapikwa.
Weusi wamefanya remix ya Afrika Mashariki ya wimbo wao Gere ambapo wamewashirikisha Navio wa Uganda na Naziz na Collo wa Kenya. Ni jana tu pia Navio ameingia studio kurekodi wimbo alioshirikishwa na Izzo Bizness.
Hiyo haitoshi.. msanii wa Uganda, Zari the Bosslady alikuja Tanzania na kufanya collabo na Diamond Platnumz.
Bado kituo cha runinga cha Maisha Magic kimeendelea kuja na vipindi vya kuwaungasha wana Afrika Mashariki zaidi. Salama Jabir ameungana na Mkenya, Malonzo kuwa hosts wa kipindi cha Tujuane Plus.
Jokate Mwegelo ameungana na staa wa Uganda, Gaitano Kagwa kuwa hosts wa show mpya, Beat the Challenge.
Kwa mifano hiyo michache, utagundua jinsi ambavyo Tanzania, Kenya na Uganda zinazidi kuwa karibu katika sekta ya burudani. Hicho ndicho kitu pekee ambacho tunaweza kufanikiwa kuwa kwenye ligi moja ya kimuziki na wasanii wa Nigeria.
Hatuwezi kuwafikia kama tutajitenga. Ushirikiano ulioneshwa na wana Afrika Mashariki baada ya kundi la Sauti Sol kuingia hatua ya pili kwenye tuzo za MTV EMA ulivutia wengi. Ushirikiano huo huo uendelee pale msanii wa Afrika Mashariki anapokuwa akishindana na wasanii wa Nigeria.
Leo hii mafanikio ya Diamond Platnumz hayasherehekiwi na Watanzania pekee. Ukiangalia comments kwenye video zake, utaona meseji nyingi kutoka kwa mashabiki wake wa Kenya wanaojivunia mafanikio yao.
Nchi za Afrika Mashariki zinaunganishwa na tamaduni nyingi lakini kikubwa ni Kiswahili ambacho kinatufanya kuwa kitu kimoja. Tukiendelea na mshikamano huu, tunaweza kutengeneza industry ya burudani kubwa itakayowanufaisha wasanii wa nchi zote. Afrika Mashariki tuendelee kuungana.