Habari

Ubunge wa Bulaya bado wang’ang’aniwa

Wapiga kura wanne wa Jimbo la Bunda waliofungua shauri kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliopita wameendelea kumng’ang’ania mbunge wa jimbo hilo, Ester Bulaya kwa kukata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu wa kutupa maombi yao.

Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Francis Kabwe alisema Jumatano hii kuwa rufaa ya wapiga kura hao, Magambo Masato, Matwiga Matwiga, Janes Ezekiel na Acetic Malagila iliyosajiliwa kwa namba 199 ya mwaka 2016, itasikilizwa mfululizo kuanzia Februari 20.

Alisema rufaa hiyo itasikilizwa jijini Mwanza na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, Salim Mbarouk, Augustine Mwarija na Shabani Lila.

Katika maombi ya msingi waliyofungua Mahakama Kuu, wapigakura hao wanaowakilishwa na Wakili Constantine Mutalemwa, wanaiomba Mahakama kutengua ushindi wa Bulaya dhidi ya aliyekuwa mgombea wa CCM, Stephen Wasira kwa madai kuwa uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka 2015 haukuwa huru na wa haki.

Pamoja na madai mengine, Masato na wenzake wanadai kuwa mchakato wa kampeni, upigaji kura na utangazaji wa matokeo uligubikwa na ukiukwaji wa sheria na utaratibu wa uchaguzi, vikiwamo vitendo vya rushwa, msimamizi wa uchaguzi kumnyima haki Wasira kwa kukataa ombi lake la kura kuhesabiwa upya.

Novemba 17, mwaka jana, Jaji Noel Chocha wa Mahakama Kuu alimtangaza Bulaya kuwa mshindi halali wa uchaguzi huo baada ya kutupilia mbali maombi ya wapigakura hao.

By: Emmy Mwaipopo

Chanzo: Mwananchi

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents