Tyga atishia kuvujisha album yake mpya, aishutumu Young Money kumfanya mateka
Bado haiko wazi kama Rapper Tyga ana beef na label yake ya Young Money (YMCMB), lakini ambacho kina uhakika ni kwamba rapper huyo ametishia kuvujisha album yake mpya kwa madai kuwa anaona kama label yake inamuwekea vikwazo vya kuitoa.
Ijumaa ya October 10, Tyga aliporomosha mvua za tweets za malalamiko, katika moja ya tweet hizo alisema album yake mpya iitwayo “The Gold Album: 18th Dynasty” imekamilika lakini label yake ambayo hakuitaja kwa jina ni kama imemfanya mateka sababu hawezi kuitoa.
Katika tweet nyingine Tyga alisema anaweza kuachana na label hiyo siku si nyingi baada ya shabiki mmoja kumuuliza kama bado yuko chini ya Young Money yenye wasanii kama Nicki Minaj, Drake na Lil Wayne.
Akiwa chini ya YMCMB, Tyga amefanikiwa kutoa album mbili ambazo ni “Careless World: Rise of the Last King” ya mwaka 2012 pamoja na “Hotel California” ya 2013.
Album yake mpya “The Gold Album: 18th Dynasty” ilipangwa kutoka November 18, 2014 lakini mpaka sasa haijawekwa wazi kama bado itatoka kwa tarehe hiyo.