Twanga Pepeta kuzindua wimbo uliotungwa na Kalala Junior
Baada ya kuondoka kwenye kundi la Mapacha Watatu na kurejea African Stars, Twanga Pepeta, muimbaji Kalala Junior ametunga wimbo mpya utakaozinduliwa hivi karibuni kama ishara ya kumkaribisha nyumbani.
Wimbo huo uitwao Nyumbani ni Nyumbani utazinduliwa sambamba na utambulisho wa muimbaji huyo aliyerudi kundini kwenye onesho maalum litakalofanyika ijumaa hii jijini Dar es Salaam.
Wiki iliyopita Kalala Junior aliwaambiwa waandishi wa habari kuwa Nyumbani ni Nyumbani ni wimbo ambao ameuandika kuzungumzia masuala mbalimbali aliyokutana nayo katika muziki mpaka kuchukua uamuzi wa kuitosa Mapacha Watatu na kurejea Twanga Pepeta.
Muimbaji huyo ambaye jina lake halisi ni Kalala Hamza Kalala, alisema ameamua kurejea Twanga Pepeta kwa mapenzi yake mwenyewe pasipo kulazimishwa na mtu kwakuwa bendi hiyo ndiyo iliyompa umaarufu.