Burudani

Serikali yafuta mchakato wa ada elekezi mashuleni

Serikali imefuta mchakato wa kutangaza ada elekezi tangu katikati ya Mei mwaka huu, ambapo udhibiti wa ada hizo sasa utafanywa na Kamishna wa Elimu na Idara ya Ukaguzi.
ndalichako

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako alisema hayo jana jioni alipokuwa akihitimisha mjadala wa bajeti ya wizara hiyo na kuongeza kuwa mchakato huo umefungwa baada ya kujadiliana na wamiliki na Kamati ya Bunge.

Kwa mujibu wa Profesa Ndalichako, usimamizi wa utoaji wa michango na ada holela katika shule hizo utashughulikiwa kwa mujibu wa sera, ambapo kutatakiwa kuwepo kwa kibali kwanza.

Alisema kutokana na hatua hiyo ya Serikali, ambayo inalenga kupata muda wa kutafakari suala hilo na kutafuta namna bora ya udhibiti, sasa hakutakuwa na ada elekezi ila michango itadhibitiwa.

Awali katika mjadala, baadhi ya wabunge walipinga mchakato huo na kutaka Serikali kujikita katika kuboresha shule zake na kuachana na utoaji wa ada elekezi. Akizungumza katika mjadala huo, Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) alisema hakuna sababu ya kuwa na ada elekezi kwa shule binafsi.

Lugola alisema kama Serikali ikitaka shule binafsi zife, ni kuwalipa vizuri walimu wake, kuwajengea nyumba zao, kuwa na madarasa na kuweka chakula na hayo yakikamilika, hakuna mtu binafsi atakayepandisha ada. Kwa mujibu wa Lugola, kama hayo hayatafanyika, kila mtu ana uamuzi wa kumpeleka mtoto katika shule anayotaka hata Ulaya.

“Kuna tatizo gani na hizi shule za binafsi? Kwanza wamerundikiwa kodi nyingi mara kupaka rangi magari na mengineyo, sasa watarudishaje hizo fedha? Ndiyo maana wanatoza ada kubwa,” alitetea.

Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Zubeda Hassan (Chadema), alielezea kushangaa ni kwa jinsi gani ada elekezi itawekwa, wakati hakuna viwango vya utoaji elimu kwa watoto. Mbunge wa Maswa, Mashimba Ndaki (CCM), alisema suala hilo la ada elekezi watakaonufaika ni watu wenye fedha kwani ndiyo wanaowapeleka watoto katika shule binafsi na kusahau kuboresha shule za Serikali ambazo ni kwa watu wenye vipato vya kawaida.

Ndaki alisema iwapo shule za Serikali zingekuwa bora, zingechukua wanafunzi wote na zile za binafsi zingekosa wateja kwa gharama zao hizo kubwa, hivyo hakuna sababu ya kuwawekea ada elekezi.

“Shule binafsi wanapata wateja kutokana na miundombinu mibovu, matatizo ya walimu yanayotokana na kutotendewa haki katika shule za Serikali tofauti na shule binafsi ambazo wanawathamini walimu na kufanya watoe elimu bora,” alisisitiza.

Alitaka waziri, badala ya ada elekezi angekuja na mkakati madhubuti wa kuboresha shule za Serikali kwa kuwapa mahitaji yao walimu, kununua vitabu mashuleni na kuboresha miundombinu na shule hizo na hilo lingesababisha wapunguze wenyewe ada zao.

Mbunge wa Viti Maalumu, Ester Mahawe (CCM) alisema Sheria ya Elimu ya 1978, inasema elimu siyo biashara bali huduma, lakini sasa wanaotoa elimu hiyo binafsi wanaonekana kama wao ni maadui.

Alisema shule binafsi, zinasaidia kusomesha Watanzania lakini bila kuthaminiwa wakati nchi nyingine watu binafsi wanasaidiwa kuwalipa mishahara, hapa nchini wanawapiga chini licha ya kuwa wanasaidia kusomesha hata watoto yatima, ili kuondoa watoto wa mitaani huku akieleza yeye katika shule yake anasomesha watoto 67.

Mahawe alisema shule binafsi wanalipa kodi zaidi ya 10, licha ya kuwa wameokoa kupeleka watoto kusomeshwa katika nchi za Kenya na Uganda huku akiomba wizara kuwapatia dawati wizarani ili wawape ushauri hususan katika mitaala.

Mbunge huyo alilalamikia shule binafsi kutengwa na wizara kwani hivi karibuni walitoa mafunzo kwa walimu wa watoto wa darasa la kwanza mkoani Dodoma bila kuwashirikisha

Source:Habari Leo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents