Ray, Irene Uwoya na Dulla (mjukuu wa Ambua) kuja na ‘Sister Marry’
Wapenzi wa filamu za Vincent Kigosi aka Ray The Greatest wanatarajia kufurahi mwezi huu baada ya muongozaji na muigizaji huyo kuwa mbioni kuachia filamu mpya iitwayo ‘Sister Marry’.
Katika filamu hiyo Ray ameigiza kama padre huku Irene Uwoya akiigiza kama mtawa ambaye alilazimishwa kuingia kwenye shughuli hiyo bila hiari yake.
Akiongea na Bongo5 leo kuhusiana na kisa kilichopo kwenye filamu hiyo, mtangazaji wa East Africa Television Abdallah Ambua aka Dulla, amesema yeye ameigiza kama Henry ambaye ni mpenzi wake na Irene Uwoya aliyeingia kwenye utawa.
Amesema filamu hiyo inajaribu kuonesha hali halisi ambapo masista wengi hujikuta wakivunja amri za utawa kwa kujihusisha na vitendo viovu ikiwa ni pamoja na kutembea na mapadre.
Dulla ameongeza kuwa Sister Marry inaweza kutoka mwezi huu ambapo Blandina ‘Johari’ Chagula naye ameigiza kama mtawa anayeitwa Sista Beata.
“Huu mzigo si mchezo subirini kwa hamu sana mara nyingi huwa sikosei kwenye kazi zangu ni sinema niliyotumia hela nyingi sana mpaka kuona hivi watu walivyo,” ameandika Ray kwenye blog yake.