Nape aunda timu ya watu wa 5 kuchunguza uvamizi wa Makonda Clouds
Waziri Habari, Utamaduni, Vijana, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, ameunda kamati Maalum ya watu watano kuchunguza kitendo kilichofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda cha kuvamia Ofisi za Clouds Media Group, kwa lengo la kushinikiza habari yake irushwe katika kipindi cha Da’ Weekend Chat Show maarufu kama (Shilawadu).
Waziri Nape amesema hayo leo wakati akizungumza na waandishi, baada ya Mkurugenzi wa vipindi na uandaaji, Rude Mutahaba kuthibitisha tukio hilo. Nape amesema kamati hiyo itafanya kazi kwa muda wa saa 24 na baada ya hapo, itatoa ripoti kwa waandishi wa habari na kila kitu kitaanikwa hadharani.
“Matukio kama haya hutokea pindi nchi inapotaka kupinduliwa, lakini kama Rais yupo na nchi haijapinduliwa basi kuingia ndani ya chombo cha habari na silaha, huku ni sawa na kunajisi uhuru wa habari katika nchi yetu,” alisema Nape
Aidha Nape amesema jambo lililotokea lisiwavunje moyo Clouds Media na wana habari kwa ujumla huku akisema kuwa serikali ipo kulinda haki za wanahabari bila kushinikizwa na lolote lililotokea.
Na Emmy Mwaipopo