Habari

Moscow: Makaburi yawekewa huduma ya Wi_Fi

Kila kukicha walimwengu wanakuja na yao, yapo yanayohuzunisha na yale yanayofurahisha kama ilivyo lengo la safu hii, ni kukuacha ukifurahi tu kama si kupigwa na butwaa.

Wakati utandawazi ukizidi kukua watu nao wanaendela kuumiza vichwa juu ya namna gani wanaweza kutumia utandawazi huo kutengeneza fedha hata kwenye maeneo ambayo awali ilikuwa ni nadra kwa watu kupoteza muda wao kama hawana kazi maalumu.

Zamani ilikuwa ni vigumu kumkuta mtu amesimama katika maeneo ya makaburi na hii ilikuwa ikiwahusu sana wale watu ambao wamekuwa na hofu ya kufa. Ndiyo maana ulikuwa ukipita katika maeneo ya makaburi unakuta kuko kimya kabisa.

Haa! Basi siyo kwa dunia hii ya leo, ichukue hii kuwa makaburi matatu yanayotembelewa sana na watu jijini Moscow yatawekewa huduma ya mtandao wa Wi-fi kwa ajili ya intaneti kwa wageni wanaotembelea hapo.

Hii ina maana kuwa watu waotembelea makaburi hayo kwa sasa wanaweza kutumia mtandao wa intaneti bila malipo katika makaburi ya Novodevichy, Troyekurovskoye na Vagankovo kuanzia mwaka huu kwa mujibu wa tovuti ya Moscow City.

Artem Yekimo ambaye ni Mkuu wa huduma za makaburi jijini Moscow, anasema lengo la kuweka huduma hiyo ni kusaidia wageni katika makaburi hayo kutafuta habari zaidi kuhusu watu mashuhuri waliozikwa humo, mbali ya kutafuta taarifa wa watu hao pia itawafanya wageni hao wafurahie matembezi yao makaburini hapo.

Kampuni ya mawasiliano ya YS System ilijitolea kuweka huduma ya wi-fi baada ya kusikia mipango ya kutenga maeneo ya watu ‘kutulia kisaikolojia’ katika makaburi hayo. Makaburi ya Novodevichy ni moja ya maeneo yanayotembelewa sana na watalii jijini Moscow.

Ambapo kati ya watu waliozikwa humo ni mwandishi Anton Chekhov, kiongozi wa zamani wa muungano wa Usovieti, Nikita Khrushchev na rais wa zamani wa Urusi, Boris Yeltsin.

By: Emmy Mwaipopo

Chanzo: Mtanzania

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents