Maisha Lounge kuzinduliwa Slipway
Albamu ya Maisha Lounge Vol 1 inatarajiwa kuzinduliwa Ijumaa Oktoba 22 kuanzia saa 12 jioni hadi saa 3 usiku katika ukumbi wa Mashua uliopo katika Hoteli ya Slipway Masaki Jijini Dar es Salaam.
Kwame Mchauru ambaye ni Meneja wa Label ya Maisha Music alipozungumza katika mkutano aliofanya na waandishi wa habari alisema kwamba albamu hii ni toleo la kwanza katika mtiririko wa matokeo mengine mbalimbali yanayotarajiwa kuandaliwa katika siku zijazo.
Kwame alisema wasanii walioshirki katika albamu hii ni pamoja na Ray C, Bi Shakila, Lord Eyes, Misoji Nkwabi, Hardmad, Carola Kinasha, Fid Q na Lufu.
Albamu hii imebeba mchanganyiko wa nyimbo tofauti na tulivu ambazo zimerekodiwa kwa vionjo vya ki-elektroniki na kuchanganywa na ladha za ala za asili za Kitanzania kama vile Ngoma, Zeze, Chalimba na Marimba.
Pia albamu hii imeshirikisha wasanii wa staili tofauti tofauti ili kufanya mseto wenye kukidhi hisia za walio wengi. Lounge ni aina ya muziki wa taratibu ambao unatumika katika maeneo mengi duniani hususan katika mahoteli makubwa na hata katika baadhi ya maofisi.
Ni aina ya muziki ambao huweza kukufariji na kukusaidia katika kuleta utulivu wa mwili na mawazo. Baada ya kuona kuwa aina ya muziki wa Lounge unaotumika hapa nchini Tanzania ni ule unaotoka katika mataifa mengine, ndipo wazo la kurekodi albamu hii likazaliwa.
Tumeamua kufanya hivi ili na sisi tuwe na muziki wa aina hii inayopigwa na kuimbwa katika mahadhi ya utaratibu tutakayojifananisha nayo kwa karibu.
Albamu hii imerekodiwa katika Studio za 41 Records na Maisha Studio chini ya prodyuza Jacob Poll na kuboreshwa nchini Denmark katika Studio za C4 pamoja na Red Red. Kazi hii imefanyika chini ya usimamizi wa Kampuni ya Maisha ya hapa Dar es Salaam.