Lundenga: Kuendesha Miss Tanzania si jambo la mchezo!
Mkurugenzi wa LINO International Agency ambao ni Waandaaji wa mashindano ya urembo ya Miss Tanzania, Hashim Lundenga amesema kuendesha mashindano hayo si kazi ndogo.
Akizungumza na Power Jams ya East Africa Radio leo, Lundenga alidai kuwa ndio maana mashindano mengine ya aina hiyo yameshindwa kudumu. Pia alitumia fursa hiyo kuwaomba radhi watanzania kwa kilichotokea hivi karibuni.
“Mashabiki wa warembo nawaomba radhi sana kwa haya yaliyotekea,” alisema.
“Mashindano haya ni magumu sana sio mashindano ya mchezo mchezo. Kuna watu wamefanya Miss East Africa, Miss Tourism wamenyang’anywa. Baraza la Sanaa la Taifa inaona kuwa huyu hawezi, kuna kashfa.”
Katika hatua nyingine Lundenga alidai kuwa kamati ya Miss Tanzania haijagombana bali watu kutoka nje ndio wanaowafanya waonekana wanagombana.
“Hatuja gombana kwenye kamati yetu,” alisisitiza.
“Watu kutoka nje wanatupiga mawe, sisi nyumba ya vioo, ukitupiga mawe lazima tubomoke na ukibomoa kuirudisha ni ngumu. Kwahiyo namna ya kuifanya tutaangalia kama inawezekana sawa, kama ikifa basi tutafanyeje.”