Kova azuia maandamano ya CUF
Jeshi la polisi kanda maalum Dar es salaam lilipokea barua yenye kumbukumbu CUF/AK/DSM/PF.0027/12a/2011/01 ya tarehe 03/06/2011 iliyosainiwa na Ndugu Shaweji Mketo, kwa niaba ya katibu mkuu wa CUF Taifa
Katika barua hiyo CUF waliomba kutaka kufanya maandamano, kwa kulaani vitendo vya polisi mkoani Mara wilaya ya Tarime, Nyamongo na mkoani Tabora wilaya ya Urambo kutokana na vifo vya watu wa kadhaa waliokufa maeneo hayo.
Akiongea kamanda wa kanda maalum ya polisi Dar es salaam, Seleman Kova, alisema madai ya CUF walitaka kuandamana toka Ubungo mataa hadi katika viwanja vya Bahresa Manzese na kufanya mkutano, kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 12 jioni.Kova amesema, ilikuhakikisha usalama uliopo unaendelea na kwa mamlaka aliyopewa kisheria za polisi anasitisha (amekataza) maandamano na mkutano huo.
Amesema sababu zilizomfanya asitishe maandamano na mkutano huo ni mashauri mbalimbali ya jinai yakiwemo hayo ya Tarime na Urambo, yameshafunguliwa mahakamani.Kwa hiyo kuruhusu maandamano na mkutano, ni sawa kuingilia uhuru wa mahakama kwakuwa katika mkutano huo watajadili mambo hayo hayo ambayo tayari yapo mikononi mwa sheria.
Sababu nyingine amesema 12 Juni mwaka huu, kutakuwa na shughuli maalum ya ugeni wa kitaifa na kimataifa, jambo ambalo linaweza kuwaweka katika hali ya ugumu katika usalama.