Jide Kupinga Fistula
Lady Jaydee ametangaza kushirikiana na CCBRT na watanzania wengine wote pande mbalimbali nchini katika kushirikiana kutatua tatizo la wagonjwa wa fistula na kujikwamua kutoka katika matatizo mbalimbali kama vile magonjwa na umasikini . Alisema hayo jana alipofanya mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Lady Jaydee alisema , ‘Ninayo furaha kuwafahamisha kuwa, mimi kama msanii ninaeangaliwa na kusikilizwa na jamii ya watu wengi pande mbali mbali za Tanzania, leo hii nimeungana na hospitali ya CCBRT kuwa shujaa wa wanawake wanaosumbuliwa na fistula na uamuzi huu umekuja baada ya CCBRT kunialika kutembelea wodi mbalimbali za wagonjwa zilizopo hospitalini hapa.
Awali aliendelea kusema, ‘Mimi binafsi niliguswa zaidi na wanawake wanaosumbuliwa na ugonjwa wa fistula, ukizingatia pia mimi ni mwanamke Nili[pata msukumo wa kusaidia kwa hali na mali kuokoa maisha ya wanawake wanaosumbuliwa na magonjwa haya.
Jay Dee alisema, ‘Tangu nizaliwe mpaka nakua mkubwa na kufikia hatua nilipo hivi sasa, nakiri sikuwahi kusikia wala kuona mgonjwa wa fistula lakini nilipotembelea hospitali ya ccbrt
nimesikitishwa zaidi baada ya kuelezwa kuwa wanawake wengi wenye ugonjwa huu hushindwa kufanya kazi wakati mwingine hata kutengwa au kujitenga na jamii zao wanazoishi kutokana na kuwa wanavuja haja ndogo au haja kubwa kila mara bila wao wenyewe kupenda wala kujijua.’
Jay Dee aliendelea kusema huu ni ugonjwa unaowapata wasichana na wanawake wakati wa kujifungua na hii hutokana na kushindwa kufika vituo vya afya vyenye huduma ya uzazi.
Fistula ni ugonjwa unaozuilika na unatibika, hakuna mwanamke anayetakiwa kuishi na fistula hasa ukizingatia ccbrt inatoa matibabu, usaifiri, chakula na malazi bure kwa wagonjwa wote wanaosumbuliwa na fistula. Nawaomba waandishi wa habari na ndugu zangu wote tujiunge kupinga Fistula katika jamii yetu.