Faraja Kotta azindua tovuti ya elimu ‘shuledirect.co.tz’
Aliyewahi kuwa mshindi wa Miss Tanzania kwa mwaka 2004, Faraja Kotta Nyalandu leo asubuhi amezindua tovuti yake maalum ambayo itajikita katika kusaidia kutoa mawazo mbadala katika kukabiliana na changamoto za kielimu kwa wanafunzi wa shule za upili lakini kwa O-Level.
Faraja alisema katika tovuti hiyo kutapatikana taarifa na habari za kielemu kwa wanafunzi kwa kuzingatia mfumo wa mtaala wa ufundishaji ambao umepitishwa, kuhakikiwa na kukubaliwa na wizara husika kama sehemu ya kuongeza chanzo ama vyanzo vya elimu Tanzania.
Kwa maneno yake anasema “vijana wa sasa wameamka na wameanza kukumbatia ama wamezoa matumizi ya teknolojia na hivyo itakuwa ni rahisi kwao kujifunza kwa kutumia mtandao huu ambao utatumia nyenzo na walimu wa shule zenye sifa Tanzania.
Aliendelea kwa kusema sababu kubwa ya kuzindua tovuti hii ni kuziba pengo la upatikanaji wa habari za kielimu ya upili na pia kuongeza maarifa, uwezo, ujuzi, kubadilishana mawazo kwa njia ya ki dijitali na kurahisisha mawasiliano kwa ukaribu baina ya wanafunzi na walimu.
Sherehe hiyo ya uzinduzi wa tovuti hiyo ya www.shuledirect.co.tz ilifanyika katika hoteli ya kimataifa ya Serena, jijini Dar-es-Slaam, na kushuhudiwa na mgeni rasmi ambaye alikuwa naibu waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi, Philip Mulugo.
Faraja aliwaomba wale wote wenye mawazo ya kuchangia ili kuboresha tovuti hiyo kuwasiliana moja kwa moja kwa kupitia namba 0752 904 152 au kwa barua pepe [email protected], skype ID ya @ShuleDirect, Twitter @ShuleDirect, Facebook ya ShuleDirect na Google + @ShuleDirect.