Habari

Dk Shein asisitiza kuwa alishinda uchaguzi kihalali

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, DK. Ali Mohamed Shein amejitetea kwamba ushindi wake ni ulikuwa halali.

shein

Akizungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Mashujaa iliyofanyika Dodoma jana, Dk. Shein alisema wapo wanaolalamikia ushindi wake na kwamba, licha ya malalamiko hayo ataendelea kufanya kazi kwa amani na Rais Dkt John Magufuli.

Hata hivyo amepiga kijembe kwamba, kelele za mlangoni hazimzuii mwenye nyumba kulala. Ingawa hakutaja moja kwa moja jina la Maalim Seif Sharif Hamad lakini bila shaka kauli hiyo inamlenga yeye (Maalim Seif) ambaye amekuwa akilalamikia kupokwa ushindi wake na kiongozi huyo wa CCM.

Safari za kutafuta haki nje ya nchi za Maalim Seif, Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) pia aliyekuwa mgombea urais visiwani humo katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana zinaonekana kuitia kiwewe CCM Zanzibar.

CCM visiwani Zanzibar imekuwa ikitoa matamko makali ikiwa ni pamoja na kutaka Maalim Seif akamatwe kwa madai ya kufanya uchochezi.

Baada ya kufutwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na kurudiwa tarehe 20 Machi mwaka huu, Maalim Seif amekuwa akiilalamikia Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kupoka ushindi wake na kumtunuku Dk. Shein.

Ndani ya nchi na katika jumuiya za kimataifa Maalim Seif amekuwa akitaka Serikali ya Dk. Shein isipewe ushirikiano wowote kwa madai ya kunyonga demokrasia.

Hata hivyo, zaidi ya mara moja Maalim Seif amekuwa akisema yeye ndiye mshindi na kwamba Wazanzibari wanatambua hivyo.

BY: EMMY MWAIPOPO

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents