Habari

Dk Shein akanusha kuwa na ugomvi na Maalim Seif

Wakati Wazanzibari leo wakiadhimisha miaka 53 ya Mapinduzi Zanzibar, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein, amesema hana ugomvi na Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye alikuwa mgombea urais kwa tiketi ya CUF katika uchaguzi mkuu wa mwaka juzi na kubainisha kuwa wanatofautiana kisiasa na kwamba ni jambo la kawaida na mazungumzo ya muafaka yalishafanyika.


Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein.

Dk Shein aliyasema hayo mjini Zanzibar Jumatano hii wakati akihojiwa na televisheni ya Azam katika kipindi cha Funguka kuhusu maandalizi ya mapinduzi, utendaji wake kama Rais wa saba Zanzibar, uchaguzi wa Zanzibar na maendeleo ya mchakato wa Katiba.

Pamoja na hayo, Rais huyo amebainisha kuwa anaamini amechaguliwa kihalali na Wanzanzibari, ambapo kufutwa na kurudiwa kwa uchaguzi wa Zanzibar mwaka 2015, hakukuwa na shinikizo lolote kutoka serikalini bali ni maamuzi ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) baada ya kubaini mchezo mchafu kwenye uchaguzi huo.

Hata hivyo alisema harakati za kuandaliwa kwa Katiba mpya ya Tanzania, zimefuata taratibu zote kwa mujibu wa Sheria na Katiba katika kipindi chake cha uongozi na Rais mstaafu Jakaya Kikwete na sasa kilichobaki ni kuendelea na mchakato wa kura za maoni na kutungwa kwa Katiba hiyo.

Aidha Dkt Shein alizungumzia Kuhusu sherehe za Mapinduzi, Rais huyo alisema Wazanzibari wanapaswa kujivunia kupatikana kwa mapinduzi hayo kwa kuwa ndio mkombozi na uhuru wao, hasa baada ya kupata mateso na manyanyaso ya kutawaliwa kutoka kwa watawala mbalimbali wakiwemo waarabu kutoka Oman.

Alisema Wazanzibari walitawaliwa tangu mwaka 1553 na Wareno kwa muda wa takribani karne mbili na baadaye Waarabu kutoka Oman kwa takribani miaka 40 hadi pale waasisi akiwemo Abeid Amani Karume, chini ya chama cha Afro Shiraz walipofanikisha mapinduzi na kuikomboa nchi hiyo.

Alisema enzi za ukoloni, Wazanzibari waliteseka ambapo pamoja na kuteswa pia walinyimwa haki ya kupata elimu, kumiliki ardhi ya nchi yao na kukosa fursa ya kupatiwa huduma muhimu za kijamii ikiwemo afya.

“Hii ni miaka 53 ya uhuru na ukombozi wa Wazanzibari, kwetu sisi mapinduzi haya ni alama yetu, ndio sifa yetu, ndio uhuru na ukombozi wetu. Mapinduzi ndio ishara na njia iliyotukomboa na kutuweka huru na sasa tunajitawala wenyewe,” alisisitiza.

BY:Emmy Mwaipopo

Chanzo: Habarileo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents