| Nzi kuasiwa Zanzibar |
|
|
|
| Friday, 27 June 2008 | |
|
Serikali imesema inatafuta njia ya kuwaasi nzi dume wanaosababisha mafunza katika matunda hususan maembe. Aliyasema ha naibu Waziri Kiongozi, Ali Juma Shamuhuna wakati alipokuwa akitoa ufafanuzi juu ya tatizo hilo, ambapo alidai kuwa kwa sasa kazi ya kuzaliana kwa nzi hao ni kubwa na ina kasi kubwa sana. Alisema katika kazi hiyo ya kuwaasi nzi hao, watashirikiana na wataalamu kutoka Nairobi na tayari wataalamu wawili kutoka Zanzibar wameshakwenda Nairobi, Kenya na wengine wawili wanatarajiwa kuungana na wenzao hivi karibuni. Akijibu swali la msingi la Mwakilishi wa Koani, Haji Mkema Haji (CCM) aliyetaka kufahamu hatua zilizochukuliwa kunusuru matunda kuendelea kuharibika kwa kuingia mafunza, Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Mazingira, Khatib Suleiman Bakari alisema mafunzo yametolewa kwa mabwana na mabibi shamba na wakulima ya namna ya kuangamiza mazalia ya mafunza hayo. “kusisitizwa kufuatwa kwa utaratibu wa uingizwaji na utoaji wa matunda nchini na tafiti mbalimbali zimefanywa katika maeneo mbalimbali” alisema. Naibu Waziri huyo alitaja baadhi ya tafiti hizo kuwa ni uwekaji wa mitego ya kunasia wadudu hao ambao tayari mafanikio yameanza kuonekana. Maeneo yaliyochaguliwa kwa utafiti huo kwa upande wa Unguja ni Uzi, Unguja Ukuu, Kilombero na Mbweni na kwa Pemba ni mchanga mdogo. Sababu za kuchagua maeneo hayo ni kwa kuzingatia idadi ya mashambulizi katika maeneo husika ikilinganishwa na maeneo mengine. Alisema kazi hiyo ilifanywa Oktoba mwaka jana na iliendelea hadi Machi mwaka huu huku mitego 546 walipewa wakulima ambapo jumla ya Nzi 2,041,114 walinaswa.
|
| < Prev | Next > |
|---|







