| Tanesco kutoa Huduma kupitia ATM za NMB |
|
|
|
| Thursday, 26 June 2008 | |
|
Shirika la Umeme Tanzania TANESCO na Benki ya NMB wamezindua huduma mpya itakayowasaidia wateja wa Tanesco ambao pia ni wateja wa benki hiyo wenye kadi za ATM, kupata huduma ya kununua umeme wa mita za LUKU. Huduma hiyo ilizinduliwa Dar es Salaam jana katika Tawi la NMB Ilala ambako ilizinduliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk. Idris Rashid na Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Ben Christiaanse. Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Christiaanse alisema kadi za ATM za benki hiyo zimetengenezwa maalum kwa ku zingatia mahitaji ya wateja na kwamba huduma hiyo mpya itawasaidia wateja kununua umeme kwa kutumia kadi badala ya kutembea na fedha. Dk. Rashid alisema wameamua kuanzishwa kwa huduma hiyo ili kupunguza usumbufu wa kupanga foleni kwa wateja wanaohitaji kupata huduma ya umeme. Ambapo alidai kuwa huduma hiyo itawasaidia wateja kwani wengi ambao hulazimika kutembea umbali mrefu ili kupata huduma ya kununua LUKU (Lipa Umeme Kadri Unavyotumia) hivyo huduma hiyo itawasaidia wateja kupata huduma ya kununua umeme saa 24 katika ATM za NMB. Christiaanse aliongeza kusema kwamba huduma hiyo itakuwa ni kwa ajili ya wateja wenye LUKU za kubofya tarakimu na itakuwa ikitolewa bure na hakutakuwa na makato ya fedha kwa malipo hayo. Aidha huduma hiyo ni moja ya mafanikio makubwa katika benki hiyo na itakuwa ikipatikana katika ATM zaidi ya 100 zilizopo nchi nzima. Akitoa maelekezo ya kutumia huduma hiyo, Christiaanse alisema mteja anatakiwa kuwa na kadi ya ATM na baada ya kuiweka katika mashine hiyo, ataingiza namba za siri na kuchagua huduma nyingine baada ya kuchagua lugha, kisha atachagua TANESCO halafu ataingiza namba za mita na kuchagua kiasi cha fedha; atathibitisha namba ya mita na kiasi cha fedha na kubonyeza ndiyo, baada ya hapo mteja ataweza kuweka umeme katika mita yake moja kwa moja.
|
| < Prev | Next > |
|---|







