Chege, Temba, na timu ya Mkubwa na Wanae kutoa msaada katika wodi ya watoto ya hospitali ya TMK
Wasanii mbalimbali wa Temeke wakiwemo Chege na Temba kutoka Wanaume Family pamoja na kundi la muziki la Mkubwa na Wanae linaloongozwa na Aslay, wanatarajia kwenda katika hospitali ya Temeke na kutoa msaada katika wodi ya watoto.
Akizungumza na Bongo5 leo, meneja wa Mkubwa na Wanae pamoja na kundi la TMK Family, Said Fela amesema wameamua kufanya hivyo ili kurudisha fadhila kwa jamii.
“Watu wa wilaya yetu wanasupport sana muziki wetu sio akina mama, vijana, wazee wote wanasupport muziki wetu,” amesema. “Kwahiyo mimi na wenzangu tukaona kumbe tunaweza kufanya kitu kwaajili ya watu wetu. Tukaona hakuna budi tulichokipata tugawane na wenzetu. Wenzetu wengine wapo mahospitalini, kwahiyo tukaona hospitali moja ambayo ipo karibu na sisi ni hii ya TMK. Tutatembelea wodi ya watoto.”
“Tumeshapewa wodi na mganga mkuu pale wodi namba mbili. Kwahiyo kesho kuanzia saa 7 akina Aslay, akina Temba na Chege tutajisikusanya na kwenda pale kujumuika na wenzetu, chetu kidogo tulicho nacho tuwagawie, we kama shukrani kwao. Haya ni maamuzi yetu kwa sababu kila tukifanya kitu kinakubalika ndani ya wilaya yetu kwahiyo na sisi inabidi turudishe vitu kwa jamii,” aliongeza Fella.
Katika hatua nyingine Fela amekanusha uvumi uliozagaa kuwa Aslay amepata mtoto hivi karibuni baada ya kuona picha akiwa na mtoto mchanga.
“Sio mtoto ya Aslay, hana mtoto,” amesema Fela.