Bomu lalipua watu Pwani
Watoto wawili wa familia moja wamejeruhiwa vibaya baada ya kulipukiwa na bomu. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Henry Salewi, amesema tukio hilo lilitokea jana mishale ya saa 2:00 usiku, katika kijiji cha Kihangaiko wilayani Bagamoyo mkoa wa Pwani.
Na Janeth Kiure, Pwani
Watoto wawili wa familia moja wamejeruhiwa vibaya baada ya kulipukiwa na bomu. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Henry Salewi, amesema tukio hilo lilitokea jana mishale ya saa 2:00 usiku, katika kijiji cha Kihangaiko wilayani Bagamoyo mkoa wa Pwani .
Amewataja watoto hao kuwa ni Monolwa Ismail, 9 na mwenzake Ngindo Ismaili, 9.
Kamanda Selewi amesema watoto hao walilipukiwa na bomu hilo wakati walipokuwa wakilichezea wakidhani ni jiwe.
Amesema waliliokota kwenye msitu wa Makindu, eneo ambalo limetengwa rasmi kwa ajili ya mazoezi ya kijeshi ya Jeshi la Wananchi la Tanzania, JWTZ.
Ameongeza kuwa awali watoto hao walikuwa wakichunga ng’ombe katika eneo hilo lakini mara wakaona bomu hilo ambapo walilichukua na kuanza kulitumia huku wakidhani ni jiwe la kuchezea.
Hata hivyo, Kamanda Selewi amesema bado haijafahamika ni aina gani ya bomu lililowalipukia watoto hao.
Kamanda Selewi amesema watoto hao wamejeruhiwa zaidi kwenye miguu na wamelazwa katika Hospitali ya Tumbi wilayani Kibaha.
Aidha kufuatia tukio hilo amewatahadharisha wananchi kutokwenda kufanya shughuli yoyote katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za kijeshi.
Source: Alasiri