Habari

Bilioni 2.4 kuboresha mradi wa maji Njombe

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema serikali imetoa shilingi bilioni 2.4 kwaajili ya kuboresha mradi wa maji katika mji wa Makambako mkoani Njombe

Ametoa kauli hiyo jana jioni (Alhamisi, Januari 19, 2017) wakati akizungumza na wananchi katika uwanja wa Polisi Makambako ulipofanyika mkutano wa hadhara akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Njombe. Waziri Mkuu alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha kila mwananchi anapata maji safi za salama katika umbali usiozidi mita 400 kama inavyosema sera ya maji.

Hata hivyo aliwataka wananchi kutofanya shughuli za kijamii katika vyanzo vya maji ili kuvilinda. Alisema Serikali inatumia fedha nyingi kutafuta maji kwa sababu vyanzo vingi zimekauka kutokana na shughuli za kibinadamu.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu alizungumzia suala la madai ya fidia kwa wananchi waliopisha ujenzi wa kituo cha ukaguzi cha pamoja na soko la kitamaifa katika eneo la Makambako aliahidi kuwa watalipwa.

“Fidia zenu mtalipwa hivi katibuni baada ya Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango kukamilisha taratibu za ulipaji,” alisema. Wananchi hao walilalamikia ucheleweshwaji wa malipo ya fidia hizo kupitia katika mabango mbalimbali pamoja na mbunge wa Njombe, Mheshimiwa Deo Sanga.

Serikali imeanzisha eneo la Idofi lililoko Makambako kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha ukaguzi wa pamoja wa magari ya mizigo ili kupunguza vikwazo vya kibiashara barabarani kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kituo hicho kitakuwa na vituo vidogo vya Polisi, Uhamiaji, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Maliasili pamoja na vituo vya mizani.

Awali mbunge wa jimbo la Njombe Mheshimiwa Sanga alisema moja ya changamoto inayowakabili wakazi wa mji wa Makambako ni ucheleweshwaji wa malipo ya fidia kwa waliopisha ujenzi wa kituo hicho hali inayosababisha baadhi yao kwenda kudai fidia hiyo kwake.

”Mheshimiwa Waziri Mkuu leo na sisi wananchi wa Makambako tutapona. Baba Majaliwa hawa wananchi wanadai fidia yao kwa muda mrefu na baadhi yao wamefikia hatua ya kuja kulala nje ya nyumba yangu wakigoma kuondoka hadi niwape ufafanuzi wa malipo yao,” alisema.

Mbali na kuwasilisha changamoto hiyo mbunge huyo pia aliishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa jitihada zake za kuboresha maendeleo ya wananchi hususan wakazi wa jimbo la Njombe.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Njombe, Bw. Christopher Ole Sendeka alisema Serikali imetenga sh. bilioni 2.8 kwa ajili ya ujenzi wa daraja la chuma lenye urefu wa mita 95 katika mto Ruhuhu.

Alisema mkataba wa ujenzi wa nguzo za daraja tayari umesainiwa kati ya mkandarasi wa kampuni ya M/s Lukolo na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa gharama ya sh bilioni 6.17 na muda wa utekelezaji ni miezi 24.

Akizungumzia mapambano dhidi ya ugonjwa wa ukimwi Bw. Ole Sendeka alisema mkoa unaendelea na kampeni za upimaji, zilizowezesha watu kufahamu afya zao na kuchukua tahadhari ya jinsi ya kujikinga na kuepuka maambukizi mapya.

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

IJUMAA, JANUARI 20, 2017.

BY: Emmy Mwaipopo

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents