Azam yamalizana na makocha wake wapya kutoka Hispania
Timu ya Azam FC imefikia makubaliano na makocha wa Hispania, Zeben Hernandez ambaye anatarajiwa kuwa kocha mkuu wa timu hiyo msimu ujao na mtaalamu wa Viungo, Jonas Garcia.
Makocha hao wamesaini mikataba ya mwaka mmoja ya kuifundisha timu hiyo kuchukuwa nafasi ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo raia wa Uingereza, Stewart Hall aliyevunja mkataba wake na timu hiyo baada ya kumalizika kwa ligi kuu msimu huu.
Afisa habari wa timu hiyo, Saad Kawemba amesema, “Tayari tumeshafikiana nao makubaliano na kila mmoja amesaini mkataba wa mwaka mmoja, kocha mkuu atakuja na benchi lake zima la ufundi kama ilivyokuwa kwa kocha aliyepita (Stewart Hall).”
Hata hivyo Kawemba ameongeza kuwa baadaye watawaongeza makocha wengine kama nafasi ya kocha msaidizi namba moja, Kocha Msaidizi namba mbili ambaye ataendelea kuwa mzawa Dennis Kitambi, daktari wa timu pamoja na kocha wa Makipa.
Mtihani wa kwanza kwa makocha hao utaanza kwenye mashindano ya kombe la Kagame yatakayoanza kutimua vumbi nchini kuanzia Julai 16 hadi Julai 30 mwaka huu.